KARIBUNI

Pata habari za kila siku, burudani,matangazo, na mengineyo mengi pia unaweza kuacha maoni yako kuhusu tovuti hii.

Thursday 7 July 2011

Polisi Mwanza yawatia mbaroni Wamachinga 131

    
Friday, 08 July 2011

WATU 131 wanaoaminika kuwa ni wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu kama Wamachinga, wametiwa mbaroni kufuatia vurugu kubwa zilizotokea juzi katika Jijini la Mwanza kusababisha uharibifu wa mali.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Simon Sirro, alisema hata hivyo baada ya kuwachambua watuhumiwa hao, polisi imebakiwa na watu 49 ambao leo watawafikisha mahakamani.

"Katika vurugu hizo watu wengine wanaweza kuwa wanapita na kukamatwa, sasa unapokamata lazima uchambue. Tulikamata watu 131 lakini baada ya kuchambua tumebaki na watu 49 ambao tumejiridhisha kuwa tunaweza kuwashtaki kutokana na kuwa na uhakika kuwa wamehusika na vurugu hizo.

Risasi zachunguzwa

Akizungumzia kujeruhiwa kwa watu hao, Kamanda Sirro alisisitiza kuwa polisi hawahusiki na kwamba hiyo inatokana na ukweli kuwa bunduki zilizotumika kuwashambulia ni zile zinazomilikiwa na Mgambo wa Jiji na si Jeshi la polisi.

"Bunduki zilizotumika kuwajeruhi Wamachinga hao ni aina ya Shotgun ambazo zinatumiwa na mgambo wa Jiji. Sasa kama walikuwa nazo mgambo kwa nini polisi tunalaumiwa," alisema.

Alisema hata hivyo polisi wanaendelea na uchunguzi wa kina kuhusu tukio hilo ili kuwabainisha watu waliohusika katika kuwajeruhi vijana hao.


Meya aruhusu Machinga

Kwa upande wake, Meya wa Jiji la Mwanza, Josephat Manyerere, alisema kutokana zoezi hilo kutohusisha ofisi yake, ameagiza Wamachinga hao kurejea katika maeneo waliyozuiliwa hadi hapo kikao cha Baraza la madiwani kitakapokutana na kupanga vinginevyo.

Alisema hali hiyo inaonyesha dharau kwa ofisi yake na mamlaka yake aliyopewa na wananchi na kubainisha kuwa hilo limetokea kutokana na kukosekana kwa mahusiano baina ya ofisi yake na ofisi ya Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza.

"Katika utendaji wetu hakuna mahusiano kabisa baina ya ofisi yangu na ya Mkurugenzi wa Jiji, haiwezekani wasaidizi wa mkurugenzi ambvaye hayupo wakatoa taarifa polisi, wakatoa taarifa kwa mkuu wa mkoa na kwa mkuu wa wilaya kwamba wataendesha zoezi la kutimua machinga wakati mie nisijuwe," alisisitiza.

Alisema kutokana na hali hiyo suala hili atalifikisha katika kikao cha Baraza la madiwani ili lijadiliwe na kuwachukulia hatua watendaji hao.

Majeruhi waliolazwa
Akizungumzia majeruhi, Mganga wa zamu katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando, Ramadhani Simba, alisema hadi majeruhi watano walikuwa bado wanaendelea kutibiwa.

Alisema majeruhi mmoja aliyemtaja kuwa ni Medard Bernard, alisharuhusiwa kurejea nyumbani.

Aliwataja wanaondelea na matibabu kuwa ni John Kulwa, Dotto Thomas, Pastory Braiton na Juma Machumu aliyelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi.

Mbunge wa Nyamagana, Ezekiel Wenje (Chadema), amesema vurugu hizo zimesababishwa na CCM kutokana na wao kuwaruhusu wafanyabiashara kufanya biashara katika maeneo ambayo amekuwa wakiwakimbiza.

Akizungumza na waandishi wa habari alisema kuwa yeye ndiye aliyewazuia Wamachinga hao kuwaondoa katika maeneo ya Jiji, jambo ambalo CCM wamekuwa wakilitumia kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza kuwatimua kwa lengo la kuonyesha kuwa Chadema kimekuwa na vurugu.

Alisema pamoja na vurugu hizo hatakubalina na mipango ya siri inayoendeshwa kwa kumtumia Mkurugenzi wa Jiji kuwahamisha Wamachinga kutoka katika maeneo ya katikati ya Jiji.

No comments:

Post a Comment