Rais JAkaya Mrisho Kikwete akizungumza na Naibu Waziri Mkuu wa Kenya na Waziri wa Fedha Mhe. Uhuru Kenyatta ambaye pia ni Mwenyekiti wa chama cha TNA, Waziri wa Sheria wa Kenya Mhe Eugene Wamalwa wa chama cha New Ford Kenya, Naibu Waziri wa Afya na mbunge wa Mombasa Mhe. Kambi Kazungu (kulia), Mbunge wa kuteuliwa wa chama cha TNA Bi Rachel Shebesh, na Mbunge wa Kajiado kwa tiketi ya TNA Moses ole Sakuda (kushoto) na mbunge wa zamani Mhe Abdullahi Alli alipokutana na ujumbe huo Ikulu jijini Dar es salaam.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh.  Jakaya Mrisho Kikwete ametaka wananchi wa Kenya wapewe nafasi ya kuamua ni viongozi gani wanawataka katika Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Machi mwakani.
Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa wananchi wa Kenya wanayo haki ya msingi kabisa kuamua hatma ya taifa lao katika Uchaguzi Mkuu huo.
Mh. rais amasema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa wabunge wa vyama mbalimbali vya siasa vya nchini Kenya uliomtembelea Ikulu jijini Dar es salaam.
Ujumbe huo uliongozwa na Naibu Waziri Mkuu wa Kenya na Waziri wa Fedha Mhe. Uhuru Kenyatta ambaye pia ni Mwenyekiti wa  chama cha TNA na Waziri wa Sheria wa Kenya Mhe. Eugene Wamalwa wa chama cha New Ford Kenya.
Wote wawili ni wagombea wa nafasi ya Urais katika uchaguzi ujao.
Wengine katika msafara huo walikuwa ni Naibu Waziri wa Afya na mbunge wa Mombasa Mhe. Kambi Kazungu, Mbunge wa kuteuliwa wa chama cha TNA  Bi. Rachel Shebesh na Mbunge wa Kajiado kwa tiketi ya TNA Moses ole Sakuda na mbunge wa zamani Mhe. Abdullahi Alli.
Rais Kikwete aliwapongeza kwa kuamua kufanya kazi kwa pamoja licha ya kuwa watakuwa washindani katika kinyang’anyiro cha uchaguzi mkuu huo.
Mh. Rais ameitakia heri nchi ya Kenya katika uchaguzi huo ujao, na kusisitiza kwamba nchi hiyo ya jirani ina umuhimu katika mustakabali wa kiuchumi kwa nchi za Afrika Mashariki.
Rais Kikwete wakati huo akiwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) alikuwa miongoni mwa viongozi walioshughulika sana kutafuta ufumbuzi wa ghasia na vurugu zilizozuka kufuatia Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2007 nchini Kenya.
Rais Kikwete alikaa siku tatu nchini Kenya akitafuta usuluhishi wa vurugu hiyo ya kisiasa nchini humo, ambayo katika mazungumzo yake ameyataja kama ajali iliyolipata Taifa la Kenya na ambayo majirani wake hawaitarajii kutokea katika uchaguzi ujao