Kamanda wa polisi mkoa wa Singida, Linuys Sinzumwa akitoa taarifa kwa waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) ya kujinyonga kwa mjasiriamali Bakari Rashid Kivite (26) kwa kile kilichodaiwa ni kulemewa na madeni makubwa.(Picha na Nathaniel Limu).
Na Nathaniel limu.
Kijana mjasiriamali mkazi wa Singida mjini Bakari Rashid  Kivite (26) amejinyonga kwa kutumia waya na kusababisha kifo chake kwa kilichodaiwa kuwa kulemewa na madeni makubwa.
Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Singida Linus Sinzumwa amesema kuwa tukio hilo la kusikitisha limetokea leo asubuhi kwenye jengo la furaha sinema.
Amesema uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa kijana huyo ambaye ni mzaliwa wa mkoa wa Iringa, alikuwa akidaiwa shilingi milioni saba na benki ya NMB tawi la Singida na wakati huo huo, alikuwa akidaiwa shilingi milioni 1.4 za pango alikokuwa akifanyia biashara yake ya kuuza maua ya kichina.
Kamada Sinzumwa amesema kijana huyo alikuwa mpangaji katika jengo la furaha sinema kwa miaka mingi, kwa hiyo akalimbikiza madai ya pango yakawa makubwa, hivyo upelelezi wa awali unaonyesha kuwa madai hayo yamechangia akatishe maisha yake.
Hata hivyo, amedai kuwa uchunguzi zaidi bado unaendelea, huku mwili wa marehemu ukiwa umehifadhiwa kwenye chumba cha maiti cha hospitali ya mkoa.
Habari zaidi kutoka eneo la tukio zinadai kuwa marehemu Bakari ameacha mke mmoja na mtoto mmoja.