Mwenyekiti wa Tanzania Women Chamber of Commerce (TWCC) Fatma Riyami (kulia) akiongea na waandishi  wa habari jijini Dar es salam juu ya Mkutano wa Saba wa Kimataifa wa Wanawake wafanyabiashara wa Nchi za Mashariki mwa Afrika unaofanyika Tanzania kwa mara ya kwanza na unaotarajiwa kufunguliwa na Makamu wa Rais wa Tanzania Dr. Mohamed Gharib Bilal. Kushoto ni Makamu wa Mwenyekiti wa TWCC Anna Matinde.
Makamu wa Rais wa Tanzania Dkt. Mohamed Gharib Bilal anakuwa Mgeni rasmi katika ufunguzi wa Mkutano wa Saba wa Kimataifa wa Wanawake wafanyabiashara wa Nchi ya Mashariki mwa Afrika unaonza leo  jijini Dar es salaam kwa lengo la kuimarisha mtandao wao.
Kauli hiyo imetolewa leo na Mwenyekiti wa Tanzania Women Chamber of Commerce (TWCC) Fatma Riyami wakati akiongea na waandishi  wa habari  Ofisi kwake.
Amesema kuwa Mkutano huo ambao ni wa saba (7) unafanyika nchini Tanzania kwa mara ya kwanza tangu walipoanzisha ushirikiano huo wa wanawake wafanyabiashara kwa nchi za Afrika Mashariki.
Mwenyekiti huyo amesema kuwa wajumbe wa Mkutano huo wanatarajiwa kutoka katika Nchi za Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Ethiopia, Sudan Kusini na mwenyeji Tanzania.
Amesema kuwa  Mkutano huo utakuwa fursa nzuri kwa wajumbe kutoka nchi zote saba kubadilishana uzoefu katika kazi ya kuwainua kiuchumi wakimama na kuimarisha Mtandao wa Wafanyabiashara wanawake katika Nchi za Afrika Mashariki.
Ameongeza kuwa hatua hiyo itasaidia kufanya soko la wafanyabiasha wanawake wa Afrika Mashariki kuwa kubwa na hivyo kuwainua kiuchumi wakimama.
Aidha Bibi Fatma Riyami amesema kuwa TWCC imeanzisha matawi katika Mikoa ya Kagera, Mwanza, Pwani, Dodoma, Mbeya, Dar es salaam na Arusha ikiwa na lengo la kutaka kuwa karibu na wafanfanyabiashara wanawake kwa nia kuimarisha Umoja wao.