Mtaalamu wa Elimu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto –UNICEF Zubeida Tumbo-Masabo akitoa ufafanuzi kuhusiana na umuhimu wa kuwa na sera madhubuti za elimu zitakazopelekea kuboresha kiwango cha elimu kuanzia ngazi za chini hadi za juu.
Na.Mwandishi wetu
Serikali ya Tanzania imeshauriwa kuwa na sera ya mpya ya elimu kwa kuwa sera iliyopo imepitwa na wakati na inasababisha mikanganyiko.
Mtaalamu wa Elimu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto –UNICEF Zubeida Tumbo-Masabo amesema upo umuhimu wa kuharakisha kutoa sera mpya ya elimu kwa sababu ndio itakayorahisisha utekelezaji badala ya kutokuwepo na sera inayo eleweka.
Aidha amesema sera zilizopo sasa zimepitwa na wakati, hivyo sera zitakazobuniwa upya zinapaswa kuwa na malengo ya kuendeleza elimu kwa watoto haswa motto wa kike.
Bi. Zubeida Tumbo-Masabo amesema vitendo vinavyofanyika sasa vya kumfukuza shule mtoto wa kike kwa mfano aliyebakwa na kupata ujauzito ni kumtia kitanzi cha maisha.
Ametumia fursa hiyo kuelezea kuwa katika sekta ya Elimu Umoja wa Mataifa unafanya shughuli za kuboresha elimu kitaifa, lakini pia inafanya kazi katika ngazi ya wilaya maalum katika kuangalia yale mambo ambayo wanayatilia mkazo na kuyachangia iwapo yamefanikiwa.
Katika wilaya hizo Umoja wa Mataifa unafanya vitu mbali mbali ambapo kama UNICEF imejikita katika kuangalia Masuala ya Upangaji Mipango, kwa kuwa mara nyingi shule nyingi hazina mipango.
Bi. Zubeida Tumbo-Masabo amefafanua kuwa shule zinapokuwa na mipango thabiti zinaweza hata kuuza mipango hiyo kwa mashirika mengine na kujipatia fedha za kuendesha shughuli zao nyingine za hapo shuleni.