Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Ali Mohamed Shein akifungua rasmini Bohari ya dawa iliopo maruhubi mjini Unguja ikiwa ni shamra shamra ya sherehe za miaka 49 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Hii ni moja ya sehemu ya ndani ya Bohari la dawa lililopo  maruhubi mjini Unguja lililozinduliwa leo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Ali Mohamed Shein.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr.Ali Mohamed Shein akimuuliza swali msambazaji dawa na vifaa tiba Bi Husna Maulid huko katika Bohari kuu ya madawa maruhubi mjini Unguja ikiwa ni shamra shamra ya sherehe za miaka 49 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Hili Ndio Bohari la madawa lililopo Maruhubi mjini Unguja lililozinduliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Ali Mohamed Shein .
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr.Ali Mohamed Shein akitoa hutuba yake ya uzinduzi wa Bohari la Madawa lililopo maruhubi mjini Zanzibar.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Mfamasia mkuu wa kwanza baada mapinduzi huko katika Bohari la madawa lililopo maruhubi mjini Zanzibar.(Picha zote na Makame Mshenga – Maelezo Zanzibar).
Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzíbar    
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema uzinduzi wa Bohari kuu ya Dawa utaiwezesha Serikali ya Mapinduzi Zanzíbar kupanga bajeti yake vyema ya dawa na kusaidia utoaji wa huduma za afya kwa ubora wa hali ya juu.
Rais shein ameyasema hayo katika hafla ya uzinduzi wa Bohari Kuu ya Dawa iliyopo Maruhubi mjini Zanzibar ikiwa ni mwendelezo wa shamra shamra za kutimiza miaka 49 ya Mapinduzi Zanzibar.
Amesema Bohari hiyo ya kisasa ni matunda ya kujivunia ya Mapinduzi ya Zanzibar ambayo kwa hakika italeta tija katika upatikanaji wa dawa na uimarisha wa afya za wananchi.
Dkt. Shein ameelezea matumaini yake kwa sekta ya afya kupitia Bohari hiyo na kwamba anaamini baada ya miaka mitatu Zanzibar itakuwa haipeleki tena Wagonjwa nje ya nchi kwa matibabu.
Aidha Dkt. Shein amewataka watumishi wa Serikali kubadilika kiutendaji kulingana na kasi ya maendeleo ikiwa ni pamoja na wafanyakazi wa Bohari hiyo kuitunza vyema ili iendelee kutoa huduma kama inavyotakiwa.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya Sira Ubwa amesema Bohari hiyo itaboresha utoaji wa huduma kwa uhakika kutokana na ubora wa vifaa na mitambo ya kisasa ambapo wataalamu wataweza kubaini mahitaji ya Dawa zinazohitajika katika kila Hospitali za Unguja na Pemba.
Kwa upande wao Mabalozi wa Marekani na Denmark wameelezea kufurahishwa kwao na juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha afya ya Wananchi hasa katika mapambano dhidi ya Ugonjwa wa Malaria na Ukimwi.
Aidha wameahidi kuendelea kutoa mashirikiano kwa Serikali hasa katika huduma za Afya kwa Mama na Watoto, Elimu,Mapambano dhidi ya magonjwa ya maambukizi pamoja na uzazi wa mpango.
Bohari hiyo iliyojengwa na Serikali ya Mapinduzi kwa msaada wa Shirika la USAID na NIDA inaelezewa kuwa ya tatu duniani katika viwango vya ubora ambapo jumla ya Dolla za Kimarekani Milion 1.2 zimetumika kukamilisha ujenzi wake.